Thursday, September 23, 2010

KIJANA WA KISASA NA KILIMO KWANZA

Kuajiriwa na kujiajiri ni changamoto kubwa zinazomkabili kijana ambaye yuko shuleni/chuoni na anatarajia kumaliza masomo yake baada ya muda mfupi. Vijana wengi wamekuwa wakifikiri waajiriwe wapi na kwa mshahara kiasi gani, katika biashara gani ambayo itawaingizia kipato cha kujikimu.
Kilimo ni moja ya shughuli rasmi ambayo kijana anaweza kujiajiri na kupata kipato. Ila ni vijana wachache ambao wamewahi kufikiri kuwa kilimo kinaweza kuwakomboa katika umaskini wa kipato. Kilimo kimedhaniwa kuwa ni shughuli inayofanywa na watu wanaoishi vijijini ambao hawajasoma na wamekosa uwelekeo katika maisha. Ndio maana mtu akiyumba katika maisha awapo mjini au akifeli shule watu humshauri aende kijijini akalime. Shughuli za kilimo zimechukuliwa kuwa ni shughuli ambayo haihitaji utaalamu. Mashuleni, mitaani na Vyouni, vijana wengi wamekuwa wakikebehi kilimo bila kujua bila kilimo wasingekuwa hapo walipo. Vijana wengi wanafikiri kufanya kazi za ofisini na wengine wanafirikiri kujiajiri katika biashara za kukaa dukani na kusubiri wateja.
Umuhimu wa kilimo unaonekana wazi kabisa kwani asilimia 80 ya watanzania wanategemea kilimo, huku kilimo kikichangia asilimia 26.7 ya pato la Taifa. Kilimo kinachangia asilimia 95 ya chakula kinachotumika nchini, asilimia 30 ya mauzo nje na asilimia 65 ya malighafi zinazotumika katika viwanda vyetu vya ndani Tanzania imejaaliwa kuwa na hekta milioni 44 za ardhi inayofaa kwa kilimo lakini ni asilimia 23 tu ndio inayotumika. Kuna hekta milioni 29 zinazofaa kwa kilimo cha umwangialiaji na maji ya kutosha yapo lakini ni asilimia 1 tu iliyo chini ya umwangialiaji. Je, hizo sio fursa kwa kijana wanaotaka kujiajiri kupitia kilimo?
Wapo vijana ambao wanajishughulisha na shughuli za kilimo, vijana hawa wamefanya shughuli hizi kwani ni mbadala baada kukosa shughuli nyingine za kufanya. Vijana hawa wamekuwa wakikabiliwa na changamoto nyingi mojawapo ya changamoto hizi ni:-

  • Ukosefu wa mtaji kulima kilimo cha kibiashara.

  • Ukosefu wa zana bora za kilimo mfano:- Matreta.

  • Wadudu waaribifu wanashambulia mazao.

  • Kilimo cha kutegemea mvua.

  • Ukosefu wa taarifa mbalimbali za kilimo na fursa zilizopo.

  • Ulanguzi wa bei sokoni baada ya kufa kwa vyama vya ushirika.
Kutokana na changamoto hizo ziko changamoto ambazo ziko ndani ya uwezo wa kijana wakisasa na zipo changamoto nyingi ambazo haziko ndani ya uwezo wa kijana.
Matatizo haya yanaweza kutatuliwa kwa:-

  • Kwanza, vijana waone kuwa shughuli za kilimo ni rasmi na kijana yeyote anaweza kujiajiri kupitia shughuli za kilimo.

  • Vijana wafahamu fursa mbalimbali zinazotokana na kilimo.

  • Serikari ichukue nafasi yake kwa kutimiza nguzo kumi za KILIMO KWANZA ambazo wamezitambulisha, nguzo hizo ni:-

  1. Utashi wa kisiasa kutoa msukumo wa mapinduzi ya kilimo

  2. Kugharamia mapinduzi ya kilimo.

  3. Uboreshaji wa mfumo wa utawala wa kilimo.

  4. Mabadaliko ya mfumo wa mkakati katika kilimo.

  5. Upatikanaji wa ardhi kwa ajili ya kilimo.

  6. Vivutio vya kuchochea uwekezaji katika kilimo.

  7. Uendeshaji wa viwanda katika kuleta mapinduzi ya kilimo.

  8. Sayansi, Technologia na Rasirimali watu katika kuwezesha mapinduzi ya kilimo.

  9. Uendesha wa miundo mbinu ili kuwezesha mapinduzi ya kilimo.

  10. Uhamasishaji na ushirikishwaji wa watanzania kuunga mkono na kutekeleza KILIMO KWANZA.
Kutokana na umuhimu huo wa kilimo vijana wa kisasa hawapaswi kupuuza shughuli za kilimo kwamba haziwafahi. Kilimo ni muhimu sana katika maendeleo ya nchi yetu kwani hutupatia chakula, ajira na hukuza pato nchini kwa ujumla.
Na. Innocent. J. Mbele
Mwenyekiti, FASO.

No comments:

Post a Comment