Thursday, May 9, 2013

Ufugaji wa nyuki ni kazi nzuri ya ziada

Ufugaji wa nyuki unaweza kuwa chanzo kizuri cha kipato cha ziada kwa wakulima wadogo wadogo.

Uzalishaji wa asali nchini Tanzania umekuwa ukitegemea sana wafugaji wadogo wadogo, wanaotumia njia za kiasili kama vile mizinga ya magogo au vyungu, kwa nyuki wa kiafrika ambao ni wengi sana kwenye mapori.


Ni muhimu kuwa na utaalamu wa kufuga nyuki


Mkulima ambae anahitaji kufuga nyuki ni lazima awe na uelewa wa mzunguko wa maisha ya nyuki. Anaye anza ni lazima aulize wafugaji wenzake ambao wana uzoefu wa kutosha, au kujiunga katika kikundi cha ufugaji ili apate ufahamu zaidi juu ya ufugaji wa nyuki.


Tafuta sehemu salama kwa ajili ya mzinga


Ni vizuri kutafuta mahali pazuri, salama, na penye sifa ya kufugia nyuki. Vifaa vyote vikishapatikana jambo linalofuata ni kuchagua mahali gani pa kuweka mzinga. Ni vizuri sehemu hii ikawa mahali ambapo makundi ya nyuki hukusanyika mara kwa mara.


Ni wapi pa kuweka mzinga!


Mara nyingine kupata eneo sahihi ni tatizo. Ni vizuri kuzingatia yafuatayo:


• Kulingana na hali ya kujilinda ya nyuki wa Afrika, haishauriwi kuweka mzinga shambani au karibu na shamba (weka umbali wa mita 150-200 kutoka kwenye mazao au nyumbani)
• Mzinga ni lazima uwekwe sehemu ambayo haitasababisha upotevu wa nyuki wanaporudi kutoka nje ya mzinga (wasiingie kwenye kundi lisilokuwa lao)
• Mizinga isiwekwe mbalimbali sana ili kuepusha usumbufu wa kutembea mbali kwa mfugaji wakati anapokagua. Eneo la kuweka mizinga ni lazima liwe :
• Kimya na mbali ya jumuia (hospitali, shule, na viwanja vya michezo) na maeneo ya biashara au viwanda.
• Karibu na maji masafi-kandokando ya mto, mabwawa ya samaki, mabeseni ya maji au sehemu ya matone.
• Iwe karibu na chakula cha nyukimimea inayochanua, miparachichi,
nazi, euculptus, migunga n.k
• Iwe sehemu ambayo ni kavu na isiwe sehemu ya tindiga kwani unyevu unyevu husababisha ugonjwa wa ukungu (fungal disease) na pia huzuia utengenezaji mzuri wa asali.
• Iwe mbali na watu waharibifu na iliyojificha kuepuka waharibifu.
• Sehemu ya mizinga ni lazima iwe inafikika kirahisi kwa kipindi chote cha mwaka ili iwe rahisi kuhamisha nyuki pale inapohitajika.
• Kuwe na kivuli cha kutosha hasa wakati wa mchana jua linapokuwa kali, na kusiwe na upepo mkali.
• Iwe mbali na mashamba, ambapo dawa za kuulia wadudu zinatumika.
Vichaka au wigo unaotenganisha mizinga na kuzuia wavamizi ni muhimu ili kupunguza ukali wa nyuki.


Jinsi ya kuweka mzinga


Baada ya sehemu ya kuweka mizinga kupatikana, kinachofuata ni kuandaa mizinga kwa ajili ya kuweka panapotakiwa.
• Safisha mzinga kuondoa uchafu wote, utando wa buibui na aina nyingine za wadudu.
• Weka chambo kwenye mzinga (waf ugaji wa nyuki mara nyingi hutumia nta) kwa kuipaka katika kuta za mzinga kwa ndani.
• Mzi nga unaweza kutundikwa kwenye mti, kwenye nguzo, kuweka kwenye jukwaa au kwenye miamba. Hii inategemea mkulima mwenyewe anapendelea njia ipi.


Aina za mizinga ya nyuki


Kifuniko juu (Top bar)


Hii ni aina ya mizinga inayotumika sana. Gharama yake ni karibi shilingi elfu hamsini za kitanzania. Ni aina nzuri sana kwa mtu anaeanza ufugaji wa nyuki kwa kuwa ni wa gharama nafuu. Hata hivyo mfugaji wa nyuki anaweza kutengeneza mzinga mwenyewe kama ana utaalamu wa useremala.


Faida


• Ni rahisi kukagua asali iliyo tayari.
• Ni rahisi kuvuna asali kuliko kuvuna toka kwenye mzinga wa kienyeji.
• Ni rahisi kuwatunza nyuki wakati wa kiangazi na inapokuwa hakuna maua. Mfugaji anaweza kuwapatia nyuki chakula ili kuongeza uzalishaji wa asali.
• Kurina asali ni rahisi sana ukilinganisha na mizinga ya magogo inayotundikwa juu ya mti, kwa kuwa haihitaji vifaa maalumu.
• Aina hii ya mizinga huwekwa kwa kuninginia jambo ambalo siyo rahisi kushambuliwa na wadudu/wanyama wanaokula asali. Inajaa haraka sana wakati ambao ni msimu wa asali kutengenezwa kwa wingi.


Hasara


• Kichane kwenye mzinga wa boksi hakina kishikizo hivyo huvunjika kwa urahisi sana kama hakitashikwa kwa uangalifu.
• Masega huvunwa pamoja na asali, jambo linalolazimu nyuki kutengeneza tena masega mengine na husababisha kupungua kwa uzalishaji wa asali.


Mzinga wa Langstroth unaweza kukupatia asali zaidi


Hii ni aina nzuri na rahisa sana ya mzinga. Pia hufahamika kama mzinga wa fremu, kwa kuwa ina fremu ambazo vichane vya masega hujishikiza. Pia una chumba kikubwa ambacho malkia hutagia mayai. Malkia anazuiliwa kuhama kwenda chumba kingine kwa kutumia waya. Kwenye chemba maalumu ya kutagia juu yake pana chemba ya kuhifadhia asali. Vichane vya masega vinatengezwa kwenye fremu na si kwenye nguzo kama ilivyo kwenye Top bar.
Ili kuvuna asali, mfugaji akiwa na masega yaliyojaa asali, hutumia vifaa maalum kwa ajili ya urinaji na kuhifadhi asali bila kupata tabu.


Langstroth ni gali kiasi fulani kwani huuzwa kuanzia kiasi cha TSh 70,000. Unaweza kuipata kutoka katika taasisi zilizopo hapo chini, taasisi na karakana binafsi, au wakala wa Serikali.
Chanzo: Mkulima Mbunifu

2 comments: