Thursday, May 9, 2013

Nyanya zinahitaji matunzo ili upate mavuno

Mkulima atapata faida kubwa ikiwa atatunza zao la nyanya kwa uangalifu mkubwa.



Nyanya huzaa vizuri sana hasa zinapowekewa mbolea mboji au samadi iliyooza vizuri. Unaweza kuongeza mbolea ya minjingu kiasi cha kijiko kimoja cha chakula au vijiko 3 vya chai kwa kila shimo. Endapo ardhi ina upungufu wa mbolea asili, inashauriwa kupanda kwanza mimea yenye uwezo wa kutoa mbolea vunde bora kama vile kunde, mucuna, soya au clotalaria kabla ya kusia mbegu za nyanya au kupanda. Epuka mbolea za viwandani kwa kuwa nitrojeni ikizidi husababisha nyanya kuvimba, na baadaye kuoza kirahisi, pia husababisha mnyanya kukua kupita kawaida. Kuwa na nitrojeni iliyozidi kwenye udongo pia husababisha majani kuwa laini sana hivyo kuvutia wadudu na magonjwa kirahisi. Ushindani wa magugu dhidi ya nyanya zako unakuwa ni mkubwa sana, hasa sehemu zenye joto na unyevu mwingi.


Ili kudhibiti magugu kwenye eneo lililo wazi, fyeka mara kwa mara na uhakikishe kuwa ni mafupi kuliko nyanya mpaka hapo nyanya zitakapokomaa na kuiva. Acha magugu uliyofyeka kwenye shamba lako yawe kama matandazo ili kusaidia kupunguza au kuzuia mmomonyoko wa ardhi, kupunguza joto kwenye ardhi na kuhifadhi unyevu kwenye udongo. Hii inaweza pia kufanywa kwa kupalilia kwa mikono katikati ya mistari ya nyanya, na kuweka matandazo hayo katikati ya mistari.


Fito


Kwa aina ya nyanya zinazorefuka sana, chomeka walau fito zenye urefu wa mita 2 katika kila mche wa nyanya na ufungie kwa kutumia kamba. Badala yake unaweza kutengeneza kichanja chenye nyaya na nguzo kila baada ya mita 1 au 2 na nyingine yenye urefu wa mita 0.15 kutoka ardhini. Funga kamba imara kwa kila mnyanya. Mnyanya unaweza kuzungushwa kwa uangalifu mkubwa kwenye kamba hiyo kulingana na unavyokuwa.


Kukatia matawi ni muhimu sana kwa aina zote za nyanya. Unaweza kuacha shina kukua na kukata matawi mawili ya awali ili kuruhusu mmea kukua vizuri. Kata matawi kulingana na mmea unavyokuwa kwa wiki. Mmea unapokuwa na viriba 6 au 8 vya maua ni vizuri kukata kichwa ili kuwezesha ukuaji mzuri matunda yatakayotokea ambayo yatakuwa na soko zuri. Majani yaliyo karibu na ardhi ni lazima yaondolewe ili kusaidia kuzuia uwezekano wa mabaka kuingia kwenye mmea na matunda. Hakuna kanuni za kukata matawi au kupata idadi flani ya matunda kwa kila mmea, hii inategemeana na mkulima na aina ya nyanya.  Nyanya zinahitaji umwagiliaji mzuri katika siku za mwanzo toka kupandwa, wakati wa kuchanua, na wakati wa kukuza matunda. Kupatikana kwa maji ya kutosha kwenye minyanya, husaidia kwa kiasi kikubwa kuwa na mazao na kukomaa kwa wakati mmoja.  Husaidia pia kupunguza uwezekano wa kuvimba na kuoza kwa nyanya, muonekano usiokuwa wa kawaida hutokana na ukosefu wa kalishamu ya kutosha wakati wa kutengeneza na kukuza matunda. Wakati wa kiangazi, ni muhimu kunyweshea angalau mara mbili kwa wiki. Unyeshaji kwa njia ya matone ni njia bora zaidi na isiyokuwa na madhara ukilinganisha na umwagiliaji wa mifereji, hii ni kwa sababu maji hudondoka kidogo kidogo kwenye shina.


Kuvuna


Nyanya kwa ajili ya kuuza zinaweza kuvunwa zikiwa bado na rangi ya kijani baada ya kukomaa, kisha zinaweza kuiva zikiwa zinasafirishwa kwenda sokoni, au zikahifadhiwa kwanza ili ziive. Nyanya zinazotumika kwa ajili ya kutengeneza supu, juisi, na mchuzi huachwa shambani mpaka ziive kiasi cha asilimia 85. Nyanya huchumwa zikiwa bado ngumu, lakini kiasi cha asilimia 65 huwa tayari kuchumwa kwa wakati mmoja.


Wadudu wa nyanya na njia za asili za kudhibiti


Sota (cutworms)


Hawa ni wadudu hatari wanaoshambulia vitalu vya nyanya. Wanakata shina la mimea iliyooteshwa au inayoota.


Ni nini cha kufanya;


• Ondoa magugu mapema, angalau wiki mbili kabla ya kupanda.
• Chimbua na utifue vizuri shamba lako kabla ya kupanda. Hii inasaidia kuwaibua sota na kufanya waliwe na maadui zao.
• Tengeneza wigo kulinda miche iliyohamishwa na kupandwa shambani. Wigo unaweza kutengenezwa kwa kuzungushia karatasi, karatasi ya foili, au ubao mwepesi kuzunguka sehemu ya bustani.
• Chimba karibu ya mimea iliyoharibiwa na uwateketeze sota.
• Wahifadhi wadudu wa asili wanaokula sota.


Vidukari (Aphids)



Vidukari hunyonya maji kwenye mimea na kusababisha mimea kupunguza uwezo wa kukua, pia hutoa ute kama asali, ambao husababisha unga unga unaosababisha mimea kukakamaa. Unga huu kwenye matunda husababisha yasipate soko.


Ni nini cha kufanya;


• Tunza wadudu wa asili wanaokula vidukari. Epuka kutumia madawa kwa wingi kwani yanaweza kuua wadudu wa asili wanaodhibiti vidukari.
• Tumia matandazo yanayong’aa. Vitu vinavyo akisi mwanga kama vile aluminiamu, husaidia vidukari wasiwezi kutua kwenye mimea.


Minyoo – (Root-knot nematodes)


Root knot huathiri sana nyanya.  Madhara yanakuwa makubwa zaidi sehemu yenye udongo wa kichanga na kunyeshea kwa kutuamisha maji. Minyoo husababisha vifundo kwenye mizizi. Mimea iliyoathiriwa hunyauka, na wakati mwingine hufa kabisa wakati wa jua.


Ni nini cha kufanya;


• Fanya mzunguko wa nyanya na nafaka.
• Usiweke kitalu cha miche mahali ambapo unahisi kuwepo magonjwa.
• Tumia aina ya nyanya inayostahimili magonjwa.
• Panda mazao mseto.
• Hakikisha kuna kiasi cha kutosha cha mbolea asili kwenye udongo.
Chanzo: Mkulima Mbunifu

No comments:

Post a Comment