Saturday, June 8, 2013

IJUE ALIZETI INAVYOTUMIKA KAMA MALISHO YA MIFUGO.


Alizeti haitoi mailisho pekee, pia inatoa mafuta bora kwa afya ya binadamu na pia malighafi inayotumiwa na nyuki kutengeneza asali.


Unapotengeneza chakula cha mifugo peke yako, si tu kupunguza gharama, lakini pia inakupa uhakika wa kuwa na chakula bora. Pia Wafugaji wa nyuki wanaopanda alizeti wanapata faida ya ziada kwa kupata asali iliyo bora kwa sababu nyuki hukusanya poleni kutoka kwenye alizeti wanapofanya ushavushaji.


Chanzo kizuri cha protini


Chakula cha mifugo kinachotengenezwa kutokana na alizeti ni chanzo kizuri cha protini kwa ajili ya mifugo, hasa ng’ombe wa maziwa, kuku, nguruwe na hata sungura. Malisho haya yana kiasi kikubwa cha protini, nyuzi nyuzi na kiasi kikubwa cha mafuta. Malisho haya yana protini kiasi cha asilimia 29-30, kiasi cha nyuzi nyuzi asilimia 27-31.


Moja ya tabia nzuri ya alizeti ni kwamba haina vitu vinavyoathiri virutubisho kwa mifugo, hata hivyo, ina kiasi kikubwa cha nyuzi nyuzi na mashudu yake kuwa magumu kiasi, jambo ambalo husababisha ugumu kidogo kwenye kusagwa tumboni. Mbali na virutubisho vya aina nyingine, alizeti ni chanzo kizuri cha kalishamu, fosiforasi na vitamini B.


Ubora wa alizeti inayotumika kwa ajili ya malisho ya mifugo inategemeana na namna ambayo imetayarishwa. Kwa mfano, alizeti inayosagwa bila kuondoa maganda ya nje, ina kiasi kikubwa cha nyuzi nyuzi (kati ya asilimia 27-30, lakini inakuwa na kiasi kidogo cha protini asilimia 23). Alizeti ambayo imetayarishwa kwa ubora wa hali ya juu huwa maganda yameondolewa na inakuwa na kiasi kikubwa cha protini, kiasi cha asilimia 40.


Mkulima anapaswa kufahamu kuwa alizeti bado inakuwa na virutubisho hata kama haitatayarishwa kwa ustadi. Mfugaji anaweza kutumia soya na karanga badala ya alizeti, lakini ni lazima apeleke alizeti kupima kuhakikisha kuwa ina nyuzinyuzi na virutubisho kwa kiwango cha nyuzinyuzi na protini kinachokubalika.


Inapendekezwa kutumia alizeti


Kulingana na utafiti ambao umefanyika nchini Tanzania, alizeti iliyochanganywa na pumba ya mahindi kwa kiasi cha asilimia 30, kisha kulishwa ng’ombe aina ya Zebu ina uwezo wa kuongeza uzalishaji wa maziwa kutoka lita 6.6 kwa siku mpaka lita 8.1 kwa siku. Nchini Zimbabwe, mashudu ya alizetu huchanganywa na mahindi pamoja na  mabua ya mahindi ambayo yamewekwa urea kwa kiwango cha wastani wa kilo 4.4 kwa siku, na kulishwa ng’ombe aina ya Jersey pamoja na ng’ombe chotara ambao hulishwa katika machungo ya wazi, Ng’ombe hawa huongeza kiasi cha maziwa kwa wastani wa kilo 5.8 mpaka kilo 6 kwa siku.


Aina ya alizeti


Kuna aina mbili za alizeti, alizeti fupi na alizeti ndefu. Aina ndefu hurefuka mpaka kufikia kiasi cha urefu wa mita 1.5-2.4. Uzalishaji wake ni hafifu ukilinganisha na mbegu za kisasa. Aina hii mara nyingi huwa ile inayojulikana kama Hungary nyeupe na Fedha. Alizeti fupi ni inayotokana na mbegu za kisasa ambayo huwa na urefu wa mita 1.2, aina hii huwa na mavuno mazuri zaidi ukilinganisha na aina ndefu.


Kutengeneza chakula cha mifugo


Kilo tatu na nusu za alizeti inapokamuliwa hutoa mafuta lita moja na mashudu kilo mbili na nusu.


Resheni kwa ng’ombe wa maziwa


•Changanya kilo 18 za mashudu ya alizeti na kilo 100 za pumba ya mahindi ili kutengeneza chakula cha ng’ombe.
•Mlishe ng’ombe anaezalisha maziwa kwa wingi kiasi cha kilo 4 ya mchanganyiko huo na kilo 2 kwa ng’ombe anaezalisha kiasi kidogo cha maziwa.
•Mbali na kulisha mchanganyiko huo, ng’ombe wa maziwa ni lazima apewe kiasi kingine cha chakula cha kawaida cha kila siku kama vile matete, hay, au aina nyingine yoyote ya malisho bora kwa kiasi cha kutosha.


Resheni kwa ajili ya kuku


Chakula cha kuanzia: Changanya kilo 22 za mashudu ya alizeti na kilo 100 za pumba ya mahindi Chakula cha kukuzia: Changanya kilo 20 za mashudu ya alizeti na kilo 100 za pumba ya mahindi au chenga.
Chakula kwa ajili ya kuku wanaotaga: Changanya kilo 18 za mashudu ya alizeti na kilo 100 za chenga za mahindi


ZINGATIA: Unapotengeneza chakula kwa ajili ya ng’ombe wa maziwa, mfugaji ni lazima ahakikishe kuwa mashudu hayazidi asilimia 20 ya resheni ya kulishia. Kwa ajili ya kulishia kuku, alizeti isizidi asilimia 7 ya jumla ya resheni.


Namna ya kuzalisha alizeti


 
Hali ya hewa: Alizeti hustawi vizuri zaidi kwenye udongo tifutifu, wenye rutuba ya kutosha. Zao hili lina mizizi inayoenda chini kwa kiwango cha kikubwa hivyo kuiwezesha kustawi hata katika sehemu yenye kiwango kidogo cha mvua. Kiasi cha wastani wa milimita 500-750 za mvua zinatosha kabisa kwa uzalishaji wa alizeti. Inaweza kulimwa kutoka usawa wabahari mpaka kufikia mwinuko wa mita 2600 kutoka usawa wa bahari.


Maandalizi ya shamba


Ni lazima kuhakikisha kuwa shamba limelimwa vizuri, ili kuweza kupata sehemu nzuri ya kusia mbegu.
Nafasi: Mbegu zinaweza kupandwa kwa nafasi ya sentimita 75 kwa 30 kwa kiasi cha kilo 2 kwa ekari moja (sawa na kilo 5 kwa hekari). Panda mbegu 3 kwa kila shimo, kisha acha mmea mmoja kwa kila shimo mimea inapofikia urefu wa sentimita 10-20.


Matumizi ya Mbolea


Alizeti hufanya vizuri kwenye udongo wenye rutuba. Matumizi ya mbolea inayotokana na miamba aina ya fosifeti inafaa zaidi kwa kuwa alizeti inahitaji fosifeti kwa kiasi kikubwa. Matumizi ya mbolea mboji iliyoandaliwa vizuri itaongeza virutubisho vya ziada kwenye udongo.
Alizeti hukua vizuri katika sehemu isiyokuwa na magugu. Palilia alizeti inapokuwa na urefu wa mita 0.7 (Kiasi cha wiki 4).


Ndege waharibifu


Ndege wanaweza kuharibu kiasi cha asilimia 50 ya alizeti endapo hawatafukuzwa. Ili kuzuia uharibifu huo, mkulima anaweza kuchukua hatua zifuatazo;
•Vunja shina la alizeti kufikia usawa wa magoti kabla ya alizeti kukauka. Unaweza pia kuvunja katika urefu wowote lakini alizeti iangalie chini ili kuzui ndege kudonoa.
• Ondoa alizeti shambani baada ya kukauka na kuihifadhi.
Ubanguaji unaweza kufanyikia nyumbani kwa kutumia fimbo
Alizeti ni lazima ikaushwe mpaka kufikia kiwango cha unyevu wa asilimia 10 kabla ya kuhifadhiwa

Chanzo:mkulima mbunifu,

No comments:

Post a Comment